
Upande wa Mashtaka katika kesi ya kutekwa kwa mfanyabiashara Mohamed Dewji ‘Mo’ umedai kuwa bado wanaendelea kuwatafuta watuhumiwa watano ili kuunganishwa katika kesi hiyo.
Wakili wa Serikali Mwandamizi, Wankyo Simon alidai hayo mbele ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu kuwa upelelezi wa shauri hilo bado haujakalima na wanaendelea kuwatafuta watuhumiwa hao watano raia wa Msumbiji na Afrika Kusini.
Watuhumiwa ni Henrique Simbue, Daniel Berdardo Manchice, Issac Tomu na Zacarious Junior wote ni raia wa Msumbiji na Phila Tshabalala raia wa Afrika Kusini.
Baada ya maelezo hayo Hakimu Mkazi Mkuu, Huruma Shaidi aliahirisha shauri hilo hadi Septemba 3, 2019.
Mshitakiwa wa kwanza katika kesi hiyo ni Dereva taxi, Mousa Twaleb(46).
Katika kesi ya msingi Twaleb alijihusisha na genge la uhalifu `anadaiwa kutenda kosa hilo kati ya Mei Mosi, 2018 na Oktoba 10, 2018 katika maeneo mbalimbali ya jiji la Dar es Salaam na Johannesburg, nchini Afrika Kusini, kwa makusudi alitoa msaada wa kutendeka vitendo vya jinai au uhalifu wa kupangwa kwa lengo la kujipatia faida.
Katika shtaka la pili, Twaleb anadaiwa, Oktoba 11, 2018 katika maeneo ya Hoteli ya Colloseum iliyopo wilayani Kinondoni jiji Dar es salaam, Twaleb pamoja na watu wengine ambao hawajafikishwa mahakamani, walimteka nyara Mohamed Dewji kwa nia ya kumhifadhi kwa siri na kumuweka maeneo ambayo ni hatari.
Katika shtaka la tatu, Wakili Simon alidai Julai 10, 2018 katika maeneo ya Mbezi Beach wilaya ya Kinondoni, mshitakiwa alitakatisha fedha kiasi cha Sh8 milioni wakati akijua fedha hizo ni zao la kosa la kushiriki genge la uhalifu.












