
Utawaambia nini mashabiki wa Simba kama kiungo wao Msudan Sharif Shiboub, yuko kwenye kikosi cha kwanza akishika dimba la katikati.
Huduma anayoitoa tangu ametua klabuni hapo inawapa mzuka na sasa mabao yake mawili kwenye ushindi wa 4-2 dhidi ya Azam, ndio umewafanya kushangilia kila anaposhika mpira.
Kiwango chake kwa sasa kimekuwa mjadala mkubwa na baadhi ya wachambuzi wa soka wanamuona Shiboub kama anakwenda kumfunika Mwamba wa Lusaka, Clatous Chotta Chama.
Mchambuzi mahiri wa soka, Ally Mayay amesema licha ya kuwa ni mapema sana kumpa Shiboub asilimia 100, lakini ni aina ya viungo wanaotakiwa katika soka la sasa.
Alisema uwezo na ubora aliounyesha kwenye mchezo dhidi ya Azam kimedhihirisha kwamba, anaweza kumfunika Chama kama ataendelea kucheza kwa kiwango hicho kwa muda mrefu.
“Sababu za kusema Shiboub amemzidi Chama kwa ubunifu, ni kuwa kwenye mchezo na Azam alionekana kila mahali anapostahili kuwepo. Alikuwa na jukumu la kukaba, kuchezesha timu na bado akafunga mabao mawili mambo ambayo Chama hawezi kuyafanya kwa wakati mmoja uwanjani,” Mayay aliliambia gazeti la Mwanaspoti
“Amecheza zaidi ya asilimia 90 na ndio kwanza anaanza kuonekana mbele ya Watanzania, hivyo tunategemea kuona ufundi mwingi kutoka kwake. Lakini, jambo la msingi asije kubweteka na kujiona amemaliza kazi, mambo ndio kwanza yanaanza”

Naye mchezaji wa zamani wa Simba, Zamoyoni Mogella alisema ameona alichokifanya Shiboub dhidi ya Azam FC, lakini akataka apewe muda zaidi kwa kuwa, kuna wachezaji wengine wana homa za vipindi.
“Nampa mechi tano zaidi na akiendelea kwa staili na kasi hiyo hiyo basi atakuwa kiboko. Ni mbunifu wa hali ya juu lakini, suala la kujiuliza ni kwamba ataendelea hivyo kwa muda mrefu? Wapo wengi walioanza kama yeye lakini, baadaye wakapotea kabisa” alisema.
Kwa upande wa Ulimboka Mwakingwe alisema Shiboub ameonyesha cheche ambazo zinatoa taswira ya nini amekuja kukifanya kwenye Ligi Kuu Bara, ingawa naye amempa muda zaidi.
“Soka la kisasa ni lile ambalo mchezaji anaweza akafanya vitu vingi kwa wakati mmoja, ndicho nilikiona kwa Shiboub ambaye aliziba hata makosa ya wengine.
“Kajiongeza kufunga si jambo dogo hilo ila swali ni je ataendeleza cheche zake, akiendeleza basi atakuwa stori ya mjini”
Mwanaspoti