
Mtendaji Mpya wa klabu ya Simba Senzo Mazingiza amewataka Wanasimba kuendelea kushirikiana ili kuifanya Simba kuwa klabu kubwa Afrika
Mazingiza ametambulishwa leo na uongozi wa Simba akichukua nafasi ya Crescentius Magori ambaye amemaliza muda wake
Akizungumza baada ya utambulisho huo uliofanyika Hotel ya Serena, Mazingiza amesema Simba ni klabu kubwa Tanzania yenye historia ya kipekee ukanda wa Afrika Mashariki
Amewataka Wanasimba kuendelea kushirikiana ili kuifanya klabu hiyo kuwa kubwa barani Afrika
“Simba ni timu kubwa sana, nimekuwa naifatilia kwa muda sasa. Nimejifunza kuwa ni timu kubwa, na tunaweza kuifanya kuwa kubwa zaidi, sio tu ukanda wa Afrika Mashariki bali kuwa klabu kubwa zaidi Afrika,” amesema
Aidha, Mazingiza ameeleza kufurahishwa na mwamko wa mashabiki wa Simba na kuwataka waendelee kuiunga mkono timu yao wakati wote
“Nilikuwa hapa simba day nilishangazwa na mashabiki wengi waliojitokeza naomba tuendelee hivi hivi siku zote tuisapoti timu”
Naye CEO aliyemaliza mda wake Crescentius Magori, amewashukuru Wanasimba wote kwa sapoti waliyompa kipindi chote alichokuwa katika nafasi hiyo
“Kuanzia wiki ijayo nitakuwa CEO mstaafu. Nawashukuru sana kwa ushirikiano mlionipa. Nawashukuru sana Wanasimba. Kwa tuliokwazana niwaombe radhi ilikuwa sababu ya kazi yangu.”














