
Uongozi wa klabu ya Yanga umemshukia beki wake Andrew Vicent ‘Dante’ ambaye amekataa kurejea kambini akishinikiza alipwe fedha anazoidai klabu hiyo
Msemaji wa Yanga Antonio Nugaz amesema pamoja na uongozi wa timu hiyo kuwa tayari kumlipa kwa awamu fedha anazodai zinazofikia Tsh Milioni 40, beki huyo amegoma kurejea kikosini
“Yanga tulikuwa tayari kumlipa kwa awamu tatu, Mil 15 mara mbili kisha kumalizia Mil 10”
“Yeye si mchezaji pekee anayeidai Yanga, wengine tumefanya nao makubaliano ya aina hiyo, wamekubali”
“Lakini Dante anaikosea Yanga kwa kuwa ameendelea kupokea mshahara bila ya kufanya kazi”
“Madai yake alipaswa kuyafanya huku akiwa kazini. Huo ndio utaratibu wa kazi mahali popote”
“Yeye kama hataki mpaka alipwe fedha zake kwa nini anaendelea kupokea mshahara wakati anajua hafanyi kazi?”
“Tayari wapo wanaohoji hatua hiyo kuwa pengine kuna mpango umejificha kama ule wa Beno, pengine dirisha dogo anataka kujiunga na timu nyingine. Sisi viongozi tunayajua ya ndani tu lakini ya huko nje nyie mashabiki mtakuwa mnayafahamu zaidi,” alisema Nugaz
Dante amegoma kujiunga kikosi Yanga akishinikiza alipwe huku mwenzie Juma Abdul ambaye alikuwa na madai, amekubali kurejea kikosini na anapokea malipo yake kwa awamu
Beki huyo kisiki hakujiunga kabisa na Yanga msimu huu akianza kwa kukosa maandalizi ya mwanzo wa msimu yaliyofanyika mkoani Morogoro