
Baada ya yale maajabu 7 ya dunia ya kale, wanasema ajabu la 8 liko Tanzania, ambalo ni Ngorongoro Crater.
Lakini nadhani hata ajabu la 9 pia linaweza kupatikana hapa hapa Tanzania; siyo kwenye utalii, bali michezo hususani soka na hasa VPL.
Maajabu haya siyo kwa vipaji vya wachezaji, bali vituko vya waamuzi. Kila siku mpya, waamuzi wetu wanakuja na maajabu mapya.
Unaweza ukajiuliza, sheria wanazotumia ni zile zile za FIFA au wana sheria zao ambazo hata TFF hawazijui…maana na wao hawakubaliani nao kabisa.
Na ndiyo sababu Rais Wallace Karia, ameagiza wadau wanaohusika na masuala ya uamuzi kukutana ili kuangalia namna ya kuboresha utendaji…hata waziri pia katoa tamko.
MAAJABU YA JANA
Ili kuamua kwamba hili ni bao au siyo bao, mwamuzi huongozwa na sheria namba 10 katika zile 17 za FIFA.
Sheria hii inasema ili lihesabike kuwa ni bao, lazima mpira WOTE uvuke mstari wa golini, katikati ya nguzo mbili na chini ya mwamba.
Endapo mwamuzi atapuliza filimbi kuashiria ni bao ilhali mpira haukuvuka mstari, basi mpira unatakiwa uanzishwe tena kwa kudundwa.
Hili la ‘mpira wote kuvuka mstari’, pia utalikuta kwenye sheria namba 9. Hii ni sheria inayohusu mpira kuwa mchezoni au la.
Inasema kwamba mpira utahesabika uko nje ya mchezo endapo WOTE utavuka mstari, aidha wa golini au pembeni.
Hapo kwenye ‘mstari wa golini’, ndipo inapomaanisha ni BAO.
KWENYE TUKIO
Mwamuzi msaidizi aliashiria kona, akiwa na maana aliuona mpira WOTE umevuka mstari. Ina maana aliona umevuka lakini siyo katikati ya nguzo mbili na chini ya mwamba?
Maana ili tumeona sheria namba 10 ikisema ili liwe bao lazima mpira uvuke mstari wa golini katikati ya nguzo mbili na chini ya mwamba.
Hapa ndo kwenye shida, mpira ulivuka mstari au haukuvuka?
Na kama haukuvuka, kwanini iwe kona?
Na kama ulivuka, ulivukia katikati ya nguzo mbili na chini ya mwamba au siyo?
Kama ni katikati ya nguzo mbili na chini ya mwamba, kwanini lisiwe bao?
Uliendelea kuwaza sana utajikuta ndiyo umeshaanza kufanya utalii wa ndani kwenye mbuga za VPL, ukishuhudia maajabu ya 9 ya dunia.
Maajabu hayatoisha Tanzania!
Cc @zakazakazi
Powered by @sports_lady_tz
#dailysporttz